Bora kuumaliza muda wangu nikitumaini,
Nikitumaini yafanyike Duniani kama mbinguni,
Mbinguni kama Duniani katika mji mpya.
Nafsi yangu imechoka kushindana na Mungu,
Kama alivyosema hatoshindana tena nami,
Kwa kuwa nimeruhusu kuwa mpumbavu.
Nimedondoka katika utukufu kwa kujitakia,
Sikumbuki nilipotoka na namna ilivyokua,
Ila kuzaliwa kwangu ilikua ni vita.
Waliniita Kashinde kwa kuwa hawakutarajia,
Walipoteza tumaini nilipowapa matumaini,
Nimezaliwa natembea sijadondoka.
Natamani sasa kuelewa kwanini nipo hapa,
Kwanini ilikua vita hata sasa bado ni vita?
Je? Nitaondoka nikiwa nimelala au ntatoweka.
Ni kweli sikiamini kifo kwa kuwa ni usingizi,
Nachoogopa ni huu mwili kuoza hainivutii,
Sipaswi kuipenda nguo hii kuliko mwili wangu.
Bado sikiamini kifo kwa kuwa ni usingizi,
Nachukia napolala nikiwa sijui kama nimelala,
Kwanini nipitiwe bila kumjua anayenipitia?
Mlalo ni mapumziko kifo ni sawa na likizo,
Mtu anayeishi ajawahi kutulia na kupumzika,
Akipumzika amekufa Je? Kifo ni Nini?
Kama ni hivyo kifo ni uzima na uzima ni kifo,
Wapumbavu tunakosa jicho la kutambua,
Kwamba atakalo lifanyike hapa kama kule.
Usijisumbue aliye juu mngoje chini sana,
Na aliye juu akungoje chini nyote ni sawa,
Paradiso ni katikati ya kuharibika na kutoharibika.
Photo Credit @thecyclopssun